Meneja wa Sunderland David Moyes ashtakiwa na FA


Meneja wa klabu ya Sunderland ya Uingereza David Moyes ameshtakiwa na chama cha soka cha Uingereza kwa utovu wa nidhamu wakati wa mechi dhidi ya Southampton Jumatano.
Southampton walishinda mechi hiyo ya Kombe EFL Cup uwanjani St Mary's kupitia bao la Sofiane Boufal. Chama cha Soka cha Uingereza (FA) kimesema inadaiwa "Moyes alitumia lugha ya kutusi au maneno ya kuudhi akiyaelekeza kwa mwamuzi wa mechi."
Kisa hicho kilitokea dakika ya 90 refa Chris Kavanagh alipokataa kuwapa Sunderland penalti baada ya mshambuliaji wa Sunderland Victor Anichebe kuonekana kuchezewa visivyo eneo la hatari.
Sunderland walilazwa 1-0. Moyes, aliyeteuliwa meneja wa Paka Weusi Julai, ameshinda alama mbili pekee kutoka kwa mechi tisa ligini.
Amepewa hadi saa tisa alasiri saa za Afrika Mashariki Jumanne kujibu tuhuma hizo.