Jeshi la Polisi pamoja na TFDA wakamata dawa bandia zenye thamani ya Sh. Mil 17 na kufunga Maduka

Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) imekamata dawa bandia aina tano katika mikoa ya Kanda ya Ziwa na Nyanda za Juu Kusini. Miongoni mwa dawa hizo ni dawa za Malaria na Vijasumu(Antibiotics). Mkurugenzi Mkuu wa TFDA, Hiiti Sillo wakati akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam amesema mamlaka hiyo ilifanya utafiti katika kanda hizo baada ya kupata taarifa za uwepo wa dawa bandia kwenye maeneo ya mikoa ya Geita na Mara katika kipindi cha mwezi Agosti na Septemba mwaka huu.



Amesema TFDA mnamo Oktoba 4 hadi 6 2016 ilifanya operesheni maalumu ya ukaguzi kwa lengo la kubaini , kukamata, kuziondoa katika soko na kuwacbukulia hatua za kisheria wanaojihusisha na biashara ya dawa bandia, za serikali, zisizosajiliwa, pamoja na dawa duni na zile zilizoisha muda wake wa matumizi.

Sirro ametaja maeneo yaliyofanyiwa ukaguzi kuwa ni pamoja na famasi, maghala ya dawa, zahanati, maduka ya dawa za mifugo na muhimu na kwamba jumla ya maeneo 207 yalifanyiwa ukaguzi.

“Uchunguzi wa awali umeonesha kuwa dawa hizi bandia zinatengenezwa hapa nchini katika makazi ya watu na maeneo mengine ya kificho ambapo zilizoisha matumizi huongezewa muda kwa kuondolewa lebo za zamani na kuwekwa mpya,”

Amesema TFDA imekamata dawa hizo bandia zenye thamani ya shilingi milioni 17.4 ambapo mkoa wa Mbeya umetajwa kuwa na idadi nyingi ya dawa hizo.

“Maduka 17 yaliyokutwa na dawa bandia na dawa za serikali yamefungwa, dawa zimekamatwa na pia inafungua majalada 38 katika vituo vya polisi dhidi ya watuhumiwa,” amesema.
Chanzo: Dewji Blog