Mbeya. Sakata la mwanafunzi Sebastian Changuku wa Shule ya Kutwa Mbeya kupigwa na walimu limechukua sura mpya

 Mbeya. Sakata la mwanafunzi Sebastian Changuku wa Shule ya Kutwa Mbeya kupigwa na walimu limechukua sura mpya baada ya walimu 18 kuhojiwa na polisi huku majalada ya watuhumiwa wanane yakitarajiwa kupelekwa kwa Mwanasheria wa Serikali kwa hatua zaidi.



Kamanda wa polisi mkoani Mbeya, Dhahiri Kidavashari amesema uchunguzi umeshafanyika kwa watuhumiwa wanane ambao ni walimu wanafunzi kutoka vyuo tofauti wanaodaiwa kuhusika na tukio hilo. “Lakini bado kuna wengine ambao tunawafuatilia jijini Dar es Salaam hivyo kufikia kesho (leo) tutakuwa tumekamilisha na kuwasilisha mafaili yao kwa Mwanasheria wa Serikali,” alisema Kamanda Kidavashari.

Amesema mwanasheria wa Serikali ndiye atatoa mwongozo kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria baada ya kupitia ripoti. “Hili suala ni pana hivyo ni umakini unahitajika katika kufanya upelelezi.

Suala la kupelekwa mahakamani litatolewa mwongozo na Mwanasheria wa Serikali baada ya kupitia ripoti ya uchunguzi,” alisema.Mkuu wa shule hiyo, Magreth Haule amethibitisha walimu wake 18 kuhojiwa na polisi kutokana na tukio la mwanafunzi huyo kushambuliwa na walimu kadhaa hivi karibuni.

#mwananchi