Mbunge Kenya aja na mbinu ya kutibu UKIMWI bila kutumia dawa


Mbunge wa Magarini katika Kaunti ya Kilifi, Harry Kombe amesema kuwa anaweza kutibu ugonjwa wa UKIMWI pamoja na magonjwa mengine bila kutumia dawa.

Kombe amesema kuwa mtu ambaye amegundulika kuwa na UKIMWI katika hatua za awali kabisa anaweza kutibiwa kwa kuchua (reflexology therapy) na hakuna dawa inayohitajika kutumika.

Licha ya Mbunge huyo kusema hivyo, Mkuu wa Baraza la Taifa la Kupambana na UKIMWI amesema kuwa hakuna dawa ya kuponya UKIWMI. Wataalamu mbalimbali wanaendelea kutafuta dawa za kutibu UKIMWI lakini hakuna mafanikio bado, alisema Vernon Mochache.

Mbunge huyo aliongeza kuwa, kuchua huko huponya watu wenye matatizo ya mshtuko wa moyo, shinikizo la damu, msongo wa mawazo, figo kushindwa kufanya kazi na matatizo ya ubongo.

Reflexology ni neno la kisayansi linalomaanisha kuchua (kusugua kwa kugandamiza) katika eneo maalum la mguu, mkono au sikio. Inaaminika kuwa sehemu hizo zinamuungano na ogani na mifumo mbalimbali za mwili  na hivyo kuzichua kunaweza kuziathiri kwa njia chanya ogani/mifumo hiyo na kuna manufaa kiafya.

Kombe amesema kuwa ameamua kutenga muda kutibu watu wengi waliojitokeza ambapo miongoni mwao ni pamoja na wabunge kutoka nchini humo.

Mbunge huyo aliyasema alipokuwa katika kampeni eneo la Chamari siku ya Jumanne na alisema kuwa alikuwa katika mpango wa kufundisha watu watakaotoa huduma hiyo ili waweze kupata ajira.

Kombe alijifunza matibabu haya kutoka kwa Mtaalamu Comulus Baya aliyejifunza kutoka Japan ambapo alisema kuchua huko husaidia kuondoa sumu mwilini. Watu wengi hasa wazee wanatumia gharama kubwa katika madawa lakini hawajui kuwa njia hii ya matibabu ni salama na ya uhakika zaidi, alisema Baya.