AANGUA KILIO MBELE YA MKUU WA MKOA "AMOSI MAKALLA."

Muuza matunda na mbogamboga wa Stendi ya Kabwe, Tumaini Japhet aliangua kilio mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla akiomba kupatiwa nafasi ya kufanyia biashara katika Soko la Mwanjelwa. Alisema amekuwa njia panda baada ya kusikia tangazo linalowatimua eneo la Kabwe, jambo ambalo litamfanya atangetange.

MKUU WA MKOA WA MBEYA


Alisema yeye ni mmoja wa waathirika wa moto uliounguza Soko la Mwanjelwa mwaka 2006.
Alidai kuwa duka lake liliungua na uongozi uliwaahidi kuwapa vyumba vya biashara baada ya soko hilo kujengwa. Japhet alisema mpaka sasa hajapatiwa eneo bali walimtaka apange kwa Sh350,000 ambazo hana. “Uuuuwiiii, mkuu wa mkoa nisaidie,’’ alisikika akilia huku akiwa amelala chini. “Mkuu wa mkoa hapa nilipo nategemewa katika familia ninaomba mnipatie kipaumbele ili niweze kumudu kuwalea watoto wangu tangu soko hilo liungue hali imekuwa mbaya katika familia yangu,” alilalamika mama huyo.

Hata hivyo, Makalla alisisitiza kuwa wafanyabiashara wote lazima wakafanyie kazi zao kwenye maeneo rasmi.
Alisema nia ya Serikali ni kuona kila mfanyabiashara wa vyakula anakuwa kwenye masoko na wenye maduka wanakuwa ndani ya vyumba badala ya kupanga bidhaa barabarani.

Mkuu huyo wa mkoa alisema Halmashauri ya Jiji la Mbeya imetenga zaidi ya maeneo 7,000 kwa ajili ya biashara katika masoko ya Isanga, Forest, Sokoine, Kabwe, Block T, Itezi, Uyole na mengine ambayo hakuyataja.
Alimuagiza mkurugenzi wa halmashauri pindi watakapoanza kugawa maeneo kwa wafanyabiashara, wampe kipaumbele muuza matunda huyo kutokana na changamoto alizonazo.