Watumishi Hewa sasa wafikia 19,629

WATUMISHI hewa 19,629 wamebainika kuwapo nchini tangu uhakiki ufanyike; na kama wangelipwa, serikali ingepoteza Sh bilioni 19.7 kwa mwezi.



Aidha, kutokana na hali hiyo, serikali imechukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi 1,663 kutoka katika taasisi zake kwa watumishi waliohusika na kuwepo kwa watumishi hewa na kati ya hizo, watumishi 638 wamefunguliwa mashtaka polisi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki, alisema bungeni mjini hapa jana kuwa serikali ingepata hasara hiyo, endapo watumishi hao hewa wangelipwa kwa mwezi.
Akitoa mfano wa halmashauri mbili, Kairuki alisema Kinondoni imekutwa na watumishi hewa 107 na kama wangelipwa ingepoteza Sh bilioni 1.279 na kwa Halmashauri ya Kishapu waligundulika 73 na wangelipwa Sh milioni 543.

Kairuki alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Maida Hamad Abdallah (CCM) aliyetaka kujua hasara serikali imeipata kwa kuwalipa watumishi hewa na adhabu kwa waliohusika na suala hilo.
Alisema, “Hadi sasa watumishi hewa 19,629 wamebainika na kama wangelipwa, kwa mwezi wangeingiza hasara ya Sh 19,749,737,180. Kuhusu adhabu na kurejesha fedha, Kairuki alisema mahakama imekuwa ikitekeleza majukumu yake na kuwatoza faini na wengine kutakiwa kurejesha fedha.

#HabariLeo