Wanafunzi vyuo vikuu waliopewa mikopo kuhakikiwa tena

BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya juu (HESLB), imetangaza mpango wa kupitia upya na kusitisha mikopo wanafunzi wote inaodai kuwa walipewa mikopo lakini hawakidhi vigezo vipya vya utolewaji wa mikopo hiyo, anaadika Charles William.

Abdul-Razaq Badru, mkurugenzi wa HESLB


Abdul-Razaq Badru, mkurugenzi wa HESLB akizungumza katika ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO jijini Dar es Salaam amewambia waandishi wa habari kuwa bodi hiyo lazima ipitie upya majina ya wanafunzi waliopewa mikopo hata kama wapo katika mwaka wao wa mwisho wa masomo.

Badru ametaja wanafunzi wanaostahili kupata mikopo kuwa ni yatima, walemavu au wenye wazazi wasiojiweza pamoja na wale wanaosoma masomo ambayo ni miongoni mwa vipaumbele vya taifa.
“Kwa vigezo hivi, muombaji anayesoma fani za sayansi za tiba na afya, ualimu wa Sayansi na Hisabati, uhandisi (Viwanda, Kilimo, Mifugo Mafuta na Gesi) au yatima, mlemavu na mwenye wazazi wenye hali duni au wasiojiweza ndiye anayestahili kupata mkopo.

HESLB tutahakiki upya wanufaikaji wa mikopo waliopo mwaka wa pili, tatu na hata wale wa mwaka wa nne ili kuondoa kila asiye na sifa na kwa wale wa mwaka wa kwanza waliokosa mikopo na wanadhani wanazo sifa wakate rufaa  kuanzia Novemba Mosi,” amesema Badru.

Wakati HESLB ikijiandaa kufanya hivyo, Kilonzo Mringo, Rais wa Serikali ya wanafunzi ya Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFMSO) amesema iwapo bodi ya mikopo itafanya hivyo, wanafunzi wengi watashindwa kuendelea na masomo.

“Mpaka sasa IFM wanafunzi wengi wana sifa na wamenyimwa mikopo, wengine wameamua kusitisha masomo yao na wengine wanasoma kwa kuja chuo wiki moja, nyingine wanaenda kutafuta fedha. Hali ni mbaya, wakiamua kupunguza tena idadi ya wanaopata mikopo basi chuo kitabaki kitupu,” amesema Mringo.

Eliudi Kasunzu, Waziri wa Mikopo katika Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (DARUSO) ameiambia MwanaHALISI Online kuwa hawapingi zoezi la uhakiki lakini wanaishangaa HESLB kuhakiki wanaopata mikopo ambao ni wachache na kuacha kuhakiki wengi walionyimwa.

“Hatuoni mantiki ya kutuhakiki tena kwa kuleta dodoso wanafunzi wajaze, fomu za maombi wanazo huko ofisini kwao wakihitaji kuhakiki basi waziangalie na si kutuingiza kwenye usumbufu wa kujaza dodoso wakati hivi karibuni wamefanya uhakiki wa idadi ya wanufaikaji.

“Hata vigezo walivyoweka mwanzo hawazingatii, tuna orodha kubwa ya wanafunzi yatima, walemavu na wanaosoma masomo yanayotajwa kuwa ni vipaumbele vya taifa lakini bado wamenyimwa mkopo halafu wanataka wachache waliopata wawapunguze zaidi,” amesema.

Boniface Emmanuel, Waziri Mkuu wa DARUSO yeye amesema anadhani kitendo cha HESLB kutaka kuhakiki wanafunzi wanaoendelea na masomo ni mbinu ya kuchelewesha kuwapa fedha zao za kujikimu.

“Kama mtu aliomba mkopo mwaka mmoja, miwili au mitatu iliyopita na akaonekana kwa bajeti na uchambuzi wa wakati huo ana vigezo vya kupata mkopo, iweje umuhakiki mwaka huu? Nadhani wanatafuta kisingizio cha kuchelewa kulipa fedha za kujikimu za awamu zijazo kwa kisingizio cha uhakiki,” amesema Boniface.