Kabila asifu mabadiliko bandarini Dar, kuanza utafiti wa kutafuta mafuta Lake Tanganyika

RAIS wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Joseph Kabila ameyasifu mabadiliko yaliyoanza kuonekana katika Bandari ya Dar es Salaam, na kuihakikishia Tanzania kuwa nchi hiyo itaongeza kasi zaidi ya matumizi ya bandari hiyo.



Hadi sasa kwa mujibu wa Rais John Magufuli, mizigo inayopitia katika bandari hiyo kutoka na kwenda DRC imeongezeka kwa asilimia 10.6 huku biashara baina ya nchi hizo ikiongezeka kutoka Sh bilioni 23 mwaka 2009 hadi Sh bilioni 396.3 mwaka jana.

Pamoja na hayo, DRC na Tanzania zimesaini rasmi mkataba wa makubaliano ya kufanya utafiti wa mafuta katika Ziwa Tanganyika, ambayo yakibainika na kuanza kuzalishwa, yatasafirishwa kupitia bomba la mafuta linalotarajiwa kujengwa kutoka Uganda kuja nchini. 

#HabariLeo