Waliotimuliwa BOT 1993 wapiga hodi kazini.

Wafanyakazi 31 waliopunguzwa katika Benki Kuu Tanzania (BoT) miaka 22 iliyopita wanatua ‘mzigo’ tena baada ya Mahakama ya Rufani kuwarejesha.



Wafanyakazi hao walifukuzwa kazi bila kufuata utaratibu wakati Serikali ilipotekeleza masharti ya upunguzaji wafanyakazi kama njia ya kurekebisha uchumi.

Wafanyakazi hao kupitia wakili wao, Barnaba Luguwa wamemwarifu Gavana wa BoT, Profesa Beno Ndulu kuhusu dhamira yao ya kurejea kazini kuanzia kesho kufuatia matokeo ya uamuzi wa Mahakama ya Rufaa.
Kiongozi wa wafanyakazi hao, Samson Magoti amesema wanakusudia kuripoti kazini Oktoba 11, 2016 ili wakapige kazi baada ya ushindi walioupata katika kesi iliyoendeshwa kwa miaka 22.

Amesema uamuzi wa jopo la majaji wa Mahakama ya Rufaa katika Shauri la Mapitio Na. 3 la 2014 lililofunguliwa na BoT dhidi yao unawawezesha kuripoti kazini baada ya kusota mahakamani kwa miaka 22.
Magoti aliwataja wenzake watakaoripoti kazini kuwa ni Nuhu Msuya, C.B. Fande, Mbaraka Katundu, Fabian Nguyeje, Omari Hassani, Alfonsi John, Audax Rugaimukamu, Ally Ndaro na Julius Haule. Wengine ni Hellen Warioba, Louis Mapunda, Yusufu Bakari, Laila Ntenja, James Chambala, E. Nyamoga, George Joseph na Simon Mashigasi. 

 #Mwananchi