Margot Gerster akutana na Hillary Clinton akitembea porini

Mwanamke mfuasi wa chama cha Democratic ambaye alivunjwa moyo na kushindwa na Bi Hillary Clinton amekutana na mtu asiyemtarajia porini, mgombea huyo mwenyewe.
Margot Gerster alienda matembezi akiwa na binti yake na mbwa katika msitu wa Chappaqua, New York.
Hakutarajia kukutana na Bi Clinton ambaye alishindwa na Donald Trump wa Reublican siku mbili awali, lakini hilo ndilo lililotokea.

Picha yake pamoja na Hillary Clinton ndiyo mara ya kwanza Bi Clinton kuonekana hadharani tangu atoe hotuba ya kukubali kushindwa Jumatano.
Bi Gerster anasema picha hiyo ilipigwa na mumewe Hillary Clinton, Bill.
Bi Gerster, ambaye huishi White Plains, amesimulia kuhusu kisa hicho kwenye Facebook.
Ujumbe wake ulipendwa mara zaidi ya 110,000 na kusambazwa na watu 9,000 kabla yake kuufanya wa faraghani.
"Nilimkumbatia na kuzungumza naye na kumwambia kwamba moja ya nyakati ninazojivunia zaidi kama mama ni wakati ambao nilimbeba Phoebe nikaenda naye na tukampigia kura," amesema.
"Alinikumbatia na kunishukuru na tukasemezana na kisha nikamwacha aendelee na matembezi."

Bi Clinton na mumewe huishi Chappaqua, wilaya ya Westchester, na ni eneo hilo ambapo Bi Clinton alipiga kura Jumanne.
Na haionekani kana kwamba hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa Bi Gerster kukutana na waziri huyo wa zamani wa mambo ya nje.
Alipakia mtandaoni picha yake na Bi CLinton, ambaye anasema alipigwa picha naye alipokuwa shule ya pili, wakati wa hafla ya kuchangisha pesa iliyoandaliwa na mamake.
Bi Clinton alikuwa mgeni wa heshima.
Chanzo: BBC