WAZIRI MKUU: Uhuru wa kuabudu kutochezewa |



WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema serikali itaendelea kulinda uhuru wa kuabudu kwa kila Mtanzania na haitamvumilia mtu wala kikundi chochote kitakachofanya mambo yanayotishia usalama na amani ya nchi.



Aidha, ametaka migogoro katika nyumba za ibada, ikiwemo misikiti imalizwe ndani kwa kutumia mabaraza badala ya kutoka nje kwa jamii kwani inaashiria sura mbaya ya kiimani na haina tija.

Majaliwa aliyasema hayo jana alipozungumza katika Baraza la Maulid ya kumbukizi ya kuzaliwa Mtume Muhammad (S.A.W) lililofanyika kitaifa kijijini Shelui wilayani Iramba, mkoani Singida na kurushwa hewani na televisheni ya TBC1.

Maulid ilisomwa juzi usiku na mapumziko pamoja na Baraza la Maulid ilikuwa jana.

Kabla ya kuzungumzia ujumbe huo kuhusu amani ya nchi, Majaliwa alimshukuru Rais John Magufuli kwa kusitisha kikao cha Kamati Kuu (CC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) isiendelee hadi jana ili kumwezesha kuhudhuria Baraza hilo la Maulid.

Waziri Mkuu alisema serikali haitayumba katika kusimamia usalama wa nchi na kuhakikisha hakuna nafasi kwa kikundi chochote kitakachoipeleka nchi pabaya na kuwataka viongozi wa dini kuwahakikisha waumini wao hawaenezi chuki dhidi ya imani nyingine.

#HabariLeo