MACHINGA NOMA WAFUNGA MITAA DAR, MADUKA YAHAMIA BARABARANI



HALI si shwari. Ndivyo tunavyoweza kusema baada ya baadhi ya mitaa katika miji iliyopo makao makuu ya mikoa mbalimbali nchini kufurika wafanyabiashara ndogondogo, maarufu ‘wamachinga’. Hiyo imetokea siku moja baada ya Rais Dk. John Magufuli kutoa agizo kwa wakuu wa mikoa na wilaya kutowafukuza maeneo ya katikati ya miji wafanyabiashara hao.



Katika miji mikuu ya mikoa, jana wamachinga walionekana wakiendelea na maandalizi ya kujenga vibanda na wengine wakipanga bidhaa zao chini.

Mapema asubuhi jana Dar es Salaam, MTANZANIA lilishuhudia mitaa kadhaa ya Kariakoo tayari wafanyabiashara hao wameweka shehena kubwa za bidhaa, huku wakiendelea kuzitandaza pembezoni na hata katikati ya barabara bila kujali wapitanjia wengine, hususani wanaotumia vyombo vya moto.

Mitaa iliyosheheni wafanyabiashara hao ni Kongo, Nyamwezi, Swahili, Sikukuu, Narung’ombe na Mchikichi.

Baadhi ya wafanyabiashara wa maduka walionekana kuduwaa, huku wengine nao wakihaha kutafuta nafasi za kutandaza bidhaa zao nje.

Wamachinga wengine walipanga bidhaa zao katikati ya barabara na kuacha sehemu ya kupita tairi za gari. Hali iliyofanya bidhaa zao kuwa uvunguni mwa gari.

Mmoja wa wamachinga walioweka bidhaa katikati ya barabara, Mtaa wa Kongo, aliyejitambulisha kwa jina moja la Robert, aliliambia MTANZANIA kuwa mtaa huo ndio wenye wateja wengi, hivyo wanalazimika kugombania nafasi za kupanga biashara zao.

Msemaji wa wamachinga wa Kariakoo, Masoud Issa, alisema wanamshukuru Rais Magufuli kwa kuwaruhusu kufanya biashara zao katikati ya miji. “Tunamshukuru na kumpongeza Rais Magufuli kwani amekuwa mtu wa mfano kwa kuwakumbuka wamachinga, ambao kwa miaka mingi tumekuwa tukionekana watu wasio na thamani wala akili,” alisema Issa.

Hata hivyo, Issa alisema ruhusa hiyo ya rais inahitajika udhibiti kwa kuwa wapo wafanyabiashara wenye maduka, ambao wanatumia agizo la rais vibaya kwa kutoa bidhaa zao madukani na kuzitandaza barabarani ili wasilipe kodi. “Kuna watu wanatafuta vijana wanatoa nje bidhaa zao madukani wanazimwaga barabarani, ambako wanajua hawatadaiwa risiri na hawatalipa kodi,” alisema Issa. #Mtanzania