Mwanafunzi ajinyonga kuondokana na kuchekwa

MWANAFUNZI wa mwaka wa kwanza aliyekuwa anachukua shahada ya ualimu Chuo cha Ajuco (zamani Chuo cha Mtakatifu Agustino, tawi la Songea) mkoani Ruvuma, Henri Mwilang’ombe (24) amejinyonga kwa kutumia nguo yake.

Ruvuma


Henri alikutwa amejinyonga kwenye kichaka majira ya mchana jana jirani na shule ya sekondari ya wasichana Songea (Songea Girls) na katika mfuko wa suruali aliyovaa ameacha ujumbe unaosema; “Nimeamua kujinyonga ili nisiendelee na mateso ninayopata kutokana na ulemavu wa mguu ambao wanafunzi wenzangu wananicheka”. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Zuberi Mwombeji alithibitisha kutokea tukio hilo.

Kamanda alisema mwanafunzi huyo amefahamika kuwa ni mwanafunzi wa chuo hicho kutokana na simu zake mbili alizokutwa nazo aina ya Nokia na baada ya Polisi kupiga baadhi ya namba watu waliopigiwa walisema ni mwanafunzi wa Ajuco.

Hata hivyo, alisema bado Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi kuhusu tukio hilo ambapo mwili wa marehemu umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Rufaa ya Songea mkoani Ruvuma. 

#HabariLeo